Arusha
Home » » WANAWAKE HALMASHAURI YA ARUSHA WATAKIWA KUTUMIA JUKWAA LA WANAWAKE KAMA CHACHU YA MAENDELEO

WANAWAKE HALMASHAURI YA ARUSHA WATAKIWA KUTUMIA JUKWAA LA WANAWAKE KAMA CHACHU YA MAENDELEO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

 
Wanawake wa halmashauri ya Arusha wilayani Arumeru wametakiwa kutumia jukwaa la uwezeshaji wanawake kiuchumi kama chachu ya maendeleo yao na wanawake wote ndani na nje ya halmashauri hiyo kwa kukaa pamoja ili kujengeana uwezo na kushirikisha fursa za maendeleo. 

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa Jukwaa la Wanawake Halmashauri ya Arusha Katibu Tawala wilaya ya Arumeru Timoth Mzava kwa niaba ya Mkuu wa wilaya ya Arumeru amesema kuwa lengo la serikali kuanzisha majukwaa hayo ni kuwakutanisha wanawake pamoja kutumia fursa ili kuchochea maendeleo ya wanawake kiuchumi kuanzia ngazi ya familia mpaka taifa na kutoa wito kuwa majukwaa hayo yatumike kwa lengo lililokusudiwa.

Amesema kuwa Jukwaa la Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi ni nyenzo muhimu kwa maendeleo ya taifa hili hivyo msiishie kuunda majukwaa tu badala yake mkatumie majukwaa haya kukabiliana na changamoto za kijamii, kiuchumi kwa kutumia fursa zilizopo katika maeneo yenu na zile zinazotolewa na serikali.

Aidha amewataka wanawake hao licha ya Jukwaa hilo kujikita kwenye masuala ya kiuchumi lakini pia kutumia majukwaa hayo kusimamia malezi bora ya watoto, kupambana na mila na desturi potofu zinzomdhalilisha mtoto wa kike pamoja na kujikita kusimamia maadili ya vijana wetu kwa maendeleo ya taifa letu.

"Jukwaa hili lisiishie kulianzisha tuu nendeni mbali zaidi tumieni Jukwaa hili kwa kuitumikia jamii yetu kwa kusimamia malezi bora hasa maadili ya vijana wetu, malezi ya watoto na familia kwa maendeleleo ya taifa letu" amesisitiza

Jukwaa hilo la halmashauri ya Arusha limekutanisha jumla ya majukwaa 27 kutoka kata zote 27 za halmashauri ya Arusha na kuwakilishwa na wajumbe watano kutoka kila kata na kufanya uchaguzi wa kuchagua viongozi wa Jukwaa la wanawake ngazi ya halmashauri.

Katika uchaguzi huo jumla ya viongozi 7 walichaguliwa kwa kupigiwa kura na mmoja aliteuliwa, hata hivyo Anna Msuya amechaguliwa kuwa Mwenyekiti,Batuli Juma Makamu Mwenyekiti, Katibu ni Grace Seneu Mollel, Katibu msaidizi Nosimu Kornelo, Mweka Hazina Asha Said na mjube wa kuchaguliwa Chiku Mohamed na mjumbe mmoja wa kuteuliwa mwakilishi walemavu ndugu Jacline Leonard na kupata jumla ya wajumbe 8 amabo watawakilisha Jukwaa hilo ngazi ya mkoa.

Akizungumza baada ya kuchaguliwa Mwenyekiti Ana Msuya amewataka wanawake wote kuweka pembeni tofauti zao ikiwemo za kidini, kisiasa hata kiuchumi ili kukabiliana na changamoto nyingi zinazowakabili wanawake wa halmashauri ya Arusha.

"Tunaposimama kwenye Jukwaa yatupasa kumuweka mwanamke kwanza, mwanamke ndio kila kitu, ili kupambana na changamoto zinazotukabili tunaweka mbali tofauti zetu pembeni kwa maendeleo yetu na taifa letu" amesema Mwenyekiti huyo.

Aidha amewashukuru kwa kumuamini na kumchagua kuwaongoza na kuwaomba kufanyakazi kwa pamoja kama timu na kusisitiza kuwa hata wale ambao hawakuchaguliwa wanathamani sawa na wanawake wote waliochaguliwa hivyo amewataka kutoa ushirikiano kwa viongozi waliochaguliwa.

Kabla ya uzinduzi wa Jukwaa hilo, wanawake hao walipewa mafunzo ya ujasiriamali na namna ya kutambua na kutumia fursa mbalimbali, majukumu ya Jukwaa la wanawake kuanzia ngazi ya kata, wilaya, mkoa mpaka taifa pamoja na ulinzi na usalama wa mtoto.

Picha za matukio ya siku hiyo.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa