Arusha
Home » » ARUMERU WASHIRIKI KUSAJILIWA VITAMBULISHO VYA TAIFA KWA STAILI YA AINA YAKE

ARUMERU WASHIRIKI KUSAJILIWA VITAMBULISHO VYA TAIFA KWA STAILI YA AINA YAKE

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

1

Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Hifadhi Hati Bi. Rose Mdami akikagua fomu ya Bwana Kitomari baada ya kukamilisha hatua ya kwanza ya usajili Vitambulisho vya Taifa kabla ya kwenda kwenye hatua ya upigaji picha. Hapa ni Kata ya Makiba kituo cha CCM Arumeru Arusha ambako zoezi hilo linafanyika.
Hawa ni Watendaji katika vitongoji viwili vya Kijiji cha Valeska wakiendelea na zoezi la kuwahakiki wananchi wao na kuwathibitisha kuwa ni wakazi halali wa eneo lao kabla ya kuwaidhinisha kupigwa picha na kuchukuliwa alama za vidole wakati wa zoezi la Usajili linaloendelea Wilayani Arumeru.
Huu ni muonekano wa nje ya jengo ambako usajili wa Vitambulisho vya Taifa unaendelea Kata yaMakiba kijiji cha Valeska. Baadhi ya wananchi wakiwa wanabadilishana mawazo huku wakisubiri kupatiwa huduma.
Afisa Usajili Wilaya ya Arumeru ndugu Edward Bujune akitoa maelezo kwa wananchi kuhusu umuhimu na faida za Vitambulisho vya Taifa wakati zoezi la kuwasajili wananchi wa Wilaya ya Arumeru likiendelea.
Meneja Mifumo ya Komputa ndugu Mohamed Mashaka akirekebisha moja ya Kamera ili iweze kufanya kazi kwa ufanisi zaidi wakati wa ziara ya kukagua utekelezaji wa zoezi la Usajili Wilayani Arumeru.
Meneja Uthibiti na Usambazaji ndugu George Mwandezi aliyeshika Kitambulisho akitoa elimu kwa wananchi kuhusu ubora wa Vitambulisho vya Taifa wakati wakiendelea na zoezi la Usajili Kata ya Makiba wakati viongozi hao walipofanya ziara kukagua maendeleo ya zoezi linaloendelea sasa katika Kata hiyo.
Mtendaji katika Kijiji cha Valeska Kata ya Makiba akihakiki fomu za wananchi kabla ya kuingia kwenye chumba cha uchukuaji alama za vidole, picha na saini ya kielektroniki. Fomu hizo zimekuwa zikusanywa na kupitiwa iwapo zimekamilika kujazwa vipengele vyote 72 vinavyohitajika
Hawa ni baadhi tu ya wananchi katika kijiji cha Valeska wakiwa kwenye foleni ya picha na uchukuaji alama za kibaiolojia wakati zoezi la Usajili likiendelea kijini hapo.


Katika hali isiyokuwa ya kawaida, wananchi katika Wilaya ya Arumeru Kata ya Makiba kijiji cha Valeska mkoani Arusha; wameonyesha kuelewa umuhimu wa Vitambulisho vya Taifa kiasi cha kujiwekea mkakati wa kuhakikisha nishati ya umeme muda wote inakuwepo ili zoezi la Usajili linaloendelea kutosimama.

Pengine hii ni tofauti na mazoea ya siku zote katika uendeshaji wa zoezi la Usajili na Utambuzi wa Watu kwa maeneo ambayo zoezi kama hilo limewahi kufanyika kiasi cha kuamsha morali zaidi kwa watumishi kutokana na mwamko mkubwa wa wananchi kushiriki zoezi hilo.

Akizungumza kwa niaba ya wananchi wa Kata hiyo; mtendaji wa Kata hiyo amesema wao kama Kata wamehamasisha wananchi kujitokeza kusajiliwa na kutokana na ushirikiano mkubwa ulioonyeshwa na wananchi wana imani Kata yao watakamilisha zoezi la Usajili ndani ya muda uliopangwa.

“Kama unavyoona hapa wananchi ndo wamekwenda wenyewe kutafuta genereta baada ya umeme kukatika na hawajashurutishwa na mtu… wamekusanyana na ghafla tunashtukia wanafunga genereta wakati tukiwa bado tunatafakari namna ya kufanya na wapi pa kupata huduma hiyo. Hii kwangu siyo kawaida kuona wananchi wakijituma hivi kwenye zoezi la kitaifa. Wananchi wana mwamko na shauku kubwa ya kuwa na Vitambulisho vya Taifa” alisema

Zoezi la kuwasajili wananchi katika Mkoa wa Arusha limeanza kwa kasi kubwa na katika Wilaya ya Arumeru zoezi hilo linaendelea katika Kata za Makiba, Maroroni na Kikwe. Usajili huu unahusisha wananchi wote wenye umri wa miaka 18 na kuendelea na unafanyikia kwenye vituo vya Usajili vilivyoanishwa na NIDA kwa kushirikiana na Uongozi wa Wilaya ya Arumeru.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa